Monday, October 1, 2012

MAHABA NIUE NI MATOKEO YA KUKOSEA VIPIMO VYA MAPENZI.


Muongozo kwamba unaweza kuingia peponi ukamkuta Firauni amestarehe ndiyo ambao unanipa sababu ya kukushauri kutokimbilia kumuacha mpenzi unayemuona haeleweki. Ushauri wangu unalenga katika eneo la kukufanya ujue vipimo vya mapenzi. Je, anakupenda kweli au anakuchezea?
Ukishajua kipimo, utajua anakufaa kwa kiasi gani. Kadhalika kama ni msumbufu, itakuwa rahisi kwako kumshusha kutoka kuwa mpenzi hadi rafiki mnafiki. Kwa maana yupo lakini kichwani kwako unamchukulia kama yupo, humwambii lakini humzingatii.
UNAISHI NAYE VIPI?
Kama mtu anavyoishi na rafiki mnafiki. Kwamba anaujua unafiki wake lakini hamwambii kwa kuhofia kuibua mambo yakawa makubwa. Ndivyo nawe unapaswa kwenda naye kwa mkondo huohuo. Muwekee kauzibe moyoni, aendelee kutuama kwenye macho na masikio yako.
Ukishamjua mtu kwamba ni rafiki yako lakini ni mnafiki, utahakikisha hajui mambo yako ya ndani. Hivyo ndivyo unavyotakiwa kufanya kwa mpenzi ambaye haeleweki. Mdhibiti kuhakikisha hatambui chochote ndani ya moyo wako. Ukimpa mwanya akakujua, atakutenda.
Unampenda kweli lakini ficha upendo wako asiuone. Wakati mwingine lazimisha kuwafanya marafiki zako wa kawaida ni bora kuliko yeye. Hiyo isiwe ni siri yako, bali fanya juu chini kumuonesha. Atakapoona, atajisikia vibaya. Hiyo ndiyo namna bora ya kumnyoosha.
Akikupigia simu, unaweza kuiacha iite mpaka ikatike. Akipiga tena, itazame hivyohivyo. Mwache apige hata mara nne. Pitisha dakika kama tano hivi, halafu mtumie SMS, muulize: “Ulikuwa unasemaje?” Ujumbe huo utamuumiza. Hujapokea, halafu umemuuliza kama hutambui nafasi yake kwako.
Jibu lako linaweza kumfanya apige tena simu, iache iite kidogo halafu pokea kisha mwambie: “Unaweza kunipigia baadaye kidogo, maana nipo nazungumza na marafiki zangu.” Ni kauli za kuumiza kwa mtu aliyekuwa anakuchukua wewe ni mwepesi au kwa lugha nyingine aliyekuwa anakuchukulia poa.
Majibu yako na jinsi ambavyo utakavyokuwa unadharau simu zake, si kumkomoa. Shabaha yako ilenge kumfanya akuheshimu. Atoke huko anapokuchukulia poa, sasa akuone nawe ni mzito. Atambue kwamba wewe una hisia kamili na hupelekwi kama ng’ombe.
Siku zote zingatia hili; Asilimia 95 ya wapenzi, wanapowaona wenzi wao wanatesekea mapenzi, hujisikia fahari kwa kujiona wao ni lulu inayopendwa. Wakati unalia, yeye atakuwa anajisifu. Sasa wewe libaini hilo mapema, badala ya kuwa mahaba niue, kuwa mwelewa kwa kukichezea kichwa chake.
Alipodhani atakukuta, aje kubaini umeshahama muda mrefu. Inawezekana kabisa wakati unafanya haya ukawa na maumivu makali ndani kwa ndani. Jambo la kufanya ni kupiga moyo konde, kwa maana unachokifanya hapo ni kwa ajili ya kutafuta amani yako ya kudumu.
Mabadiliko yako ya tabia, yatamfanya mnyonge kwako. Wakati anakuwa mkali kutokana na vitendo vya kumpuuza unavyomuonesha, wewe endelea kumuonesha kwamba hujali. Atajiuliza maswali mengi lakini mwisho ataingiwa na mawazo kuwa umempata mtu mwingine ndiyo maana huna habari naye.
Endelea kutokumjali. Mwache ajilimbikize maswali ambayo hayana majibu sahihi kwa upande wake. Akikuuliza kama una mtu mwingine, usimpe jibu la moja kwa moja. Atakuona katili lakini hiyo ndiyo tiba yako. Kinyume chake, atakugeuza punda kwa kufanya kile anachokitaka.

No comments:

Post a Comment